Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Pwani, Nsajigwa George, amezitaka asasi za kiraia na mashirika yasiyo ya kiserikali (NGOs) kufanya kazi kwa kuzingatia sheria, kanuni, uwazi na uwajibikaji ili kuongeza tija katika utoaji wa huduma kwa jamii.
Nsajigwa ametoa kauli hiyo Juni 26 wakati akifungua Mkutano wa Jukwaa la Mashirika yasiyo ya Kiserikali Mkoa wa Pwani, uliofanyika katika Ukumbi wa mdogo wa Mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Pwani.
Katika hotuba yake, alisisitiza umuhimu wa mashirika hayo kuzingatia taratibu za kisheria katika utekelezaji wa majukumu yao, hasa kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.
“Mwaka2025 ni mwaka wa uchaguzi. Naomba niagize kuwa mashirika yote yafanye kazi kwa kuzingatia sheria na kanuni. Msibadilike na kuwa sehemu ya migawanyiko ya kisiasa au Uchochezi. tunawategemea katika kulinda amani na utulivu, ambayo ni tunu ya taifa,” alisema Nsajigwa.
Aidha,alieleza kuwa mashirika hayo ni wadau muhimu wa Serikali katika kusukuma gurudumu la maendeleo, kuimarisha ustawi wa jamii, na kutekeleza malengo ya Dira ya Maendeleo ya Taifa pamoja na mikakati ya kupunguza umaskini.
Katika hatua nyingine alimuagiza Msajili Msaidizi wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali Mkoa wa Pwani, Grace Tete, kuhakikisha anakusanya changamoto, mapendekezo na michango ya mashirika hayo kwa lengo la kuyafanyia kazi kwa pamoja ili kuboresha utoaji wa huduma zenye tija.
Kwa upande wake, Mwakilishi kutoka Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, ambaye pia ni Afisa Ufuatiliaji na Tathmini Mkuu kutokaOfisi ya Msajili wa NGOs, Charles Komba, alisisitiza umuhimu wa utoaji wataarifa sahihi za kifedha na idadi ya walengwa waliowafikiwa kwenye ngazi yamkoa, pamoja na kujenga uhusiano thabiti na wafadhili.
“Serikali imetambua umuhimu wa mashirika haya na imeweza kuandaa miongozo mbalimbali ikiwemo Mwongozo wa Mchango wa NGOs, pia ushirikishwaji wao katika vikao vya ngazi ya kata, wilaya na mkoa, pamoja na kuandaa mfumo wa usajili wakielektroniki wenye ufanisi zaidi,” alisema Komba.
Naye Mwenyekiti wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali Mkoa wa Pwani, Prisca Ngweshem,alishukuru Serikali kwa ushirikiano unaoendelea kutolewa na kuahidi kuendeleza mashirikiano hayo, hususan katika utoaji wa elimu kwa jamii, huduma bora na takwimu sahihi, ili kuchangia maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani
Sanduku la Posta: 30080 Kibaha
Simu ya Mezani: 023 2402287/2402500
Simu ya Mkononi: 023 2402287/2402500
Barua pepe: barua@pwani.go.tz
Hakimiliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Haki zote zimehifadhiwa.