Mkuu wa Wilaya ya Rufiji, Luteni Kanali Fredrick Faustin Komba, amewahimiza wananchi pamoja na watumishi wa Mkoa wa Pwani kutekeleza kwa vitendo maono ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, hususan katika sekta ya kilimo.
Amesema wananchi wanapaswa kutumia kikamilifu fursa zilizopo katika mkoa huo kwa lengo la kujikita kwenye kilimo chenye tija na kuimarisha ushindani chanya miongoni mwao, ili kuongeza uzalishaji na hatimaye kuufanya Mkoa wa Pwani kuwa kinara wa kilimo cha mazao ya ufuta, mbaazi, korosho na choroko hapa nchini.
Luteni Kanali Komba alitoa kauli hiyo jana kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani, katika mkutano wa wadau wa tasnia ya ufuta na mbaazi uliofanyika katika ukumbi wa FDC uliopo Ikwiriri, wilayani Rufiji, mkoani Pwani. Mkutano huo uliandaliwa na Chama Kikuu cha Ushirika Mkoa wa Pwani (CORECU).
“Tuzitumie fursa zote zilizopo kama vile ardhi, mbolea na nguvu kazi ya watu wetu ili kuongeza uzalishaji. Tushindane kwa uzalishaji bora kati yetu ili Mkoa wa Pwani uwe mfano wa kuigwa na mikoa mingine nchini,” alisema Mheshimiwa Luteni Kanali Komba.
Aidha, alisema kuwa Serikali imefanya juhudi kubwa kuwawezesha wakulima, hasa katika upatikanaji wa mbolea na masoko ya uhakika ya ndani na nje ya nchi, kwa lengo la kuongeza kipato cha wakulima na kuchochea ukuaji wa uchumi.
Katika hatua nyingine, aliwataka Wakurugenzi wa Halmashauri za Mkoa wa Pwani kujikita katika kilimo cha mazao yote ya biashara yanayolimwa katika mkoa huo, na kuepuka ubaguzi wa mazao, kwa kuwa ardhi ya mkoa huo inaruhusu kilimo cha aina mbalimbali.
Vilevile, aliwahimiza wakulima kujiepusha na uuzaji holela wa mazao yao, na kusisitiza matumizi ya mfumo wa stakabadhi ghalani pamoja na mizani ya kidigitali kupitia Vyama vya Msingi (AMCOS), kuanzia hatua za awali. Alisisitiza pia umuhimu wa kila mmoja kuwa mlinzi wa mwenzake katika kulinda maslahi ya wakulima.
Kwa upande wake, Mrajisi Msaidizi wa Mkoa wa Pwani, Bw. Mutaabazi, alipokuwa akitoa mwongozo wa mauzo ya ufuta na mbaazi kwa msimu wa mwaka 2025/2026, alisema kuwa Vyama vya Msingi vya Ushirika pamoja na watunza maghala wanapaswa kuzingatia viwango na ubora wa mazao kwa kuweka madaraja kuanzia ngazi ya mkulima. Pia alisisitiza matumizi ya mizani ya kisasa pamoja na utoaji wa risiti kwa kila muamala, ili kuweka kumbukumbu sahihi kwa wakulima.
Naye Meneja Mkuu wa CORECU, Bw. Hamis Mantawela, akiwasilisha taarifa ya maandalizi ya ukusanyaji na uuzaji wa ufuta na mbaazi kupitia mfumo wa stakabadhi ghalani kwa msimu wa mwaka 2025/2026, alisema kuwa maandalizi ya vitabu vya mazao (shajala) yamekamilika na vinapatikana katika ofisi za CORECU makao makuu Kibaha, tawi la Kibiti, na katika ofisi ya Chama cha Msingi Kigoma AMCOS wilayani Mkuranga.
Aliongeza kuwa, kwa upande wa vifungashio, CORECU imeratibu upatikanaji wa magunia 400,000 yenye uwezo wa kuhifadhi tani 20,000 za ufuta na mbaazi, pamoja na kusambaza mizani 135 ya kidigitali kwa AMCOS zote zinazokusanya mazao, ambapo kila chama kimepatiwa angalau mzani mmoja.
Akitoa taarifa ya uzalishaji, Afisa Kilimo wa Mkoa wa Pwani, Bw. Jerry Abel, alisema kuwa kwa mwaka wa kilimo 2024/2025, mkoa uliweka lengo la kuzalisha tani 22,000 za ufuta na tani 500 za mbaazi, lakini uzalishaji halisi ulikuwa tani 13,053 za ufuta na tani 298 za mbaazi.
Kuhusu mipango ya kuongeza uzalishaji kwa msimu ujao, Bw. Abel alisema kuwa CORECU itaendelea kusambaza mbegu bora za ufuta na mbaazi, wakati Halmashauri zitaendelea kutoa elimu kupitia mashamba darasa, kusimamia usambazaji wa mbegu bora, na kuhakikisha upatikanaji wa masoko pamoja na kuanzisha mashamba ya mbegu ili kuongeza tija.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani
Sanduku la Posta: 30080 Kibaha
Simu ya Mezani: 023 2402287/2402500
Simu ya Mkononi: 023 2402287/2402500
Barua pepe: barua@pwani.go.tz
Hakimiliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Haki zote zimehifadhiwa.