Kamati ya Amani ya Mkoa wa Pwani imewahimiza wananchi kuendelea kudumisha umoja, upendo na utulivu kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, ikisisitiza umuhimu wa kulinda amani kabla, wakati na baada ya uchaguzi.
Kamati hiyo inayojumuisha viongozi wa Dini mbalimbali Mkoani humo imektana na waandishi wa habari leo Oktoba 28, 2025 na kutoa taarifa yao ya pamoja.
Mwenyekiti Mwenza wa Kamati hiyo, Mchungaji Julius Shemkai wa Kanisa la KKKT, alisisitiza umuhimu wa utulivu siku ya kupiga kura na kuwataka wananchi kujiepusha na vitendo vinavyoweza kuleta vurugu.
“Tujiepushe na maandamano yasiyoruhusiwa, uharibifu wa vituo vya kupigia kura au mikusanyiko isiyo halali,” alisema Mchungaji Shemkai.
Aliwapongeza wagombea na vyama vya siasa kwa kuendesha kampeni kwa amani na ustaarabu katika kipindi cha miezi miwili ya kampeni, bila kutumia lugha za matusi au chuki.
Mchungaji Shemkai pia aliwahimiza wapiga kura kujitokeza kwa wingi siku ya uchaguzi, kutumia haki yao ya kidemokrasia kumchagua Rais, Mbunge na Diwani, na baada ya kupiga kura kurejea majumbani au kuendelea na shughuli zao wakisubiri matokeo kwa utulivu.
Naye Mwenyekiti Mwenza wa Kamati hiyo, Sheikh Khamis Mtupa, alitoa wito kwa Watanzania wote kujiweka mbali na uchochezi wa aina yoyote unaoweza kuhatarisha amani ya nchi.
“Tupuuze maneno na vitendo vya uchochezi vinavyolenga kuvuruga uchaguzi na utulivu wa taifa letu. Tanzania ibaki salama kabla na baada ya uchaguzi,” alisema Sheikh Mtupa.
Amesema kila Mtanzania ana jukumu la kulinda amani, akisisitiza kuwa hakuna sababu ya mtu kumzuia mwingine kutumia haki yake ya kikatiba ya kupiga kura.
“Hatuna nchi nyingine ya kwenda kuishi. Uchaguzi ni haki ya kila raia, hivyo asitokee yeyote kumzuia mwingine kutumia haki hiyo kwa sababu binafsi,” aliongeza Mtupa.
Akiendelea, Sheikh Mtupa aliwasihi wasimamizi wa uchaguzi kuhakikisha wanatenda haki kwa vyama vyote na wagombea, ili kudumisha imani ya wananchi katika mchakato wa uchaguzi.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani
Sanduku la Posta: 30080 Kibaha
Simu ya Mezani: 023 2402287/2402500
Simu ya Mkononi: 023 2402287/2402500
Barua pepe: barua@pwani.go.tz
Hakimiliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Haki zote zimehifadhiwa.