Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhe. Abubakar Kunenge, ameagiza mamlaka husika kuhakikisha mafunzo ya udereva kwa maafisa usafirishaji (bodaboda) yanatolewa katika mkoa mzima, na kwamba wahitimu wapatiwe leseni mara tu baada ya kukamilisha mafunzo hayo.
Agizo hilo limetolewa leo, Novemba 30, wakati Mhe. Kunenge akizindua mafunzo ya Udereva kwa maafisa usafirishaji wa Wilaya ya Kisarawe yanayofanyika katika ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya. Amesisitiza kuwa ni muhimu maafisa hao kuwa wazalendo, kulinda amani ya nchi na kuonesha mfano bora wa utendaji kazi ili kuipa heshima Serikali na kumuenzi Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.
“Nyinyi ni wasomi na wadau wakubwa wa uchumi katika nchi yetu. Kwa mujibu wa Katiba, kulinda usalama wa nchi ni wajibu wa kila raia. Uzalendo ni kujiuliza umeifanyia nini nchi yako, siyo imekufanyia nini,” alisema Mhe. Kunenge.
Kwa upande wake, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, ACP Salim Morcase, amewataka maafisa hao kuunda na kusajili vikundi mara baada ya kupata leseni ili kukidhi vigezo vya kupatiwa mikopo ya asilimia 10. Pia aliwapongeza kwa ushirikiano wao na viongozi katika kutatua changamoto mbalimbali, huku akiwahimiza kuwa mabalozi wa amani na kuepuka matumizi mabaya ya mitandao.
Naye Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Pwani, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi Edson Mwakihaba, amewahakikishia washiriki kuwa leseni zao zitatolewa kwa haraka mara tu watakapokamilisha mafunzo.
Akizungumza mbele ya wakufunzi, Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe, Mhe. Petrol Magoti, amewataka maafisa usafirishaji hao kufanya kazi kwa bidii ili kujikwamua kiuchumi, akibainisha kuwa Serikali imeweka mazingira mazuri ya kuwawezesha kufikia malengo hayo. Pia amesema anaendelea kufanyia kazi ombi lao la kupatiwa shamba kwa ajili ya kuanzisha shughuli za kilimo zitakazochangia kuongeza kipato chao.
Akitoa ufafanuzi kuhusu mafunzo hayo, Katibu Tawala wa Wilaya ya Kisarawe, Sara Ngwele, amesema kuwa hii ni awamu ya pili ya mafunzo, ambapo awamu ya kwanza ilifanyika Novemba 22, 2025 na ilihusisha maafisa usafirishaji 228, huku awamu ya pili ikiwa na washiriki 250. Mafunzo hayo yanatolewa na wakufunzi kutoka Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) pamoja na VETA.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani
Sanduku la Posta: 30080 Kibaha
Simu ya Mezani: 023 2402287/2402500
Simu ya Mkononi: 023 2402287/2402500
Barua pepe: barua@pwani.go.tz
Hakimiliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Haki zote zimehifadhiwa.