Timu ya madaktari bingwa 64 walioko chini ya mpango maalum wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, imewasili mkoani Pwani kwa ajili ya kutoa huduma za kibingwa katika halmashauri zote za mkoa huo, pamoja na kubadilishana ujuzi wa kitaalamu na watumishi wa afya walioko katika vituo mbalimbali.
Mratibu wa timu hiyo kutoka Wizara ya Afya, Bw. Joachim Masunga, amesema kuwa ujio wa madaktari hao, ambao ni wa mara ya tatu mkoani humo, unalenga kupunguza changamoto zinazowakabili wakazi wa Pwani ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakilazimika kusafiri umbali mrefu hadi Hospitali ya Taifa ya Muhimbili ili kupata huduma za kibingwa.“Kwa kuwaleta madaktari hawa karibu na wananchi, tunalenga kupunguza gharama na usumbufu wa usafiri wa wagonjwa pamoja na kuimarisha huduma za afya katika mkoa huu,” alisema Masunga.
Madaktari hao watakuwa mkoani Pwani kwa kipindi cha siku tano na wamesambazwa katika hospitali za halmashauri zote tisa za mkoa, ili kuhakikisha huduma zinawafikia wananchi kwa usawa na kwa wakati.
Akizungumza baada ya kuwapokea madaktari hao, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Dkt. Kusirie Ukio, alisema kuwa ujio wa timu hiyo ni hatua muhimu katika kuboresha huduma za afya na kupunguza idadi ya rufaa zinazotumwa Hospitali ya Taifa Muhimbili.
“Kwa muda mrefu tumekuwa tukilazimika kuwapeleka wagonjwa Dar es Salaam kwa ajili ya huduma za kibingwa. Ujio wa madaktari hawa utasaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza rufaa hizo na kuleta unafuu kwa wagonjwa na familia zao,” alisema Dkt. Ukio.
Mpango huu ni sehemu ya jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita kuhakikisha kuwa huduma bora za afya zinapatikana hadi ngazi ya msingi, na kwamba kila Mtanzania anapata huduma stahiki bila vikwazo vya kijiografia au kiuchumi.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani
Sanduku la Posta: 30080 Kibaha
Simu ya Mezani: 023 2402287/2402500
Simu ya Mkononi: 023 2402287/2402500
Barua pepe: barua@pwani.go.tz
Hakimiliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Haki zote zimehifadhiwa.