Mkuu wa Wilaya ya Kibaha, Mhe. Nickson Simon, amefungua mafunzo elekezi kwa madiwani wa Halmashauri za Wilaya ya Kibaha na Chalinze yaliyofanyika leo Januari 15, 2026, katika Ukumbi wa Mikutano uliopo Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Mhe. Nickson amewataka madiwani kuwa mabalozi wazuri wa usimamizi wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika kata zao, akisisitiza umuhimu wa uwajibikaji, uadilifu na ufuatiliaji wa karibu wa miradi hiyo ili kuhakikisha inaleta tija kwa wananchi.
Amebainisha kuwa amekuwa na utaratibu wa kutoa zawadi kwa madiwani wanaofanya vizuri katika kusimamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo, hatua inayolenga kuwahamasisha viongozi hao kutekeleza majukumu yao kwa bidii na weledi.
“Madiwani mnapaswa kuwa wakali katika kufuatilia utekelezaji wa miradi na sheria za Halmashauri kwa kutumia takwimu sahihi, lakini msijenge ukali kwa watu au kushughulikia masuala binafsi,” amesema Mhe. Nickson.
Aidha, amewasisitiza madiwani kutumia lugha ya staha wanapotekeleza majukumu yao ya uongozi, akieleza kuwa lugha ya kiongozi ni msingi wa kujenga mahusiano mazuri kati ya viongozi, wataalamu na wananchi.
“Chuki na hasira zisihitimishe mazungumzo yenu na Wakurugenzi pamoja na wataalamu. Kosoeni miradi, siyo watu,” amesisitiza.
Pia amewahimiza madiwani kujifunza kujishusha na kujipandisha kulingana na mazingira ya uongozi, akibainisha kuwa kiongozi bora anatambua wakati wa kuwa kiongozi na wakati wa kuwa raia wa kawaida na amewataka kujiepusha na tamaa ya kujinufaisha na mali za umma, kukubali kukosoa na kukosolewa, pamoja na kufanya kazi kwa ushirikiano bila ubaguzi wa kisiasa kwa maslahi ya wananchi.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani
Sanduku la Posta: 30080 Kibaha
Simu ya Mezani: 023 2402287/2402500
Simu ya Mkononi: 023 2402287/2402500
Barua pepe: barua@pwani.go.tz
Hakimiliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Haki zote zimehifadhiwa.