Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani imeanza maandalizi ya maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika kwa kufanya kikao maalum cha maandalizi kilichofanyika leo katika ukumbi wa rasilimali (Resource Center) uliopo katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Kibaha Pwani.
Mgeni rasmi katika kikao hicho alikuwa Katibu Tawala Msaidizi Mipango na Uratibu, Edina Katalaiya.
Wajumbe wa kikao hicho walikubaliana kuwa kilele cha maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika kwa ngazi ya mkoa mwaka huu kitafanyika katika Halmashauri ya Mji Kibaha.
Akizungumza katika kikao hicho, Afisa Maendeleo ya Jamii wa Mkoa wa Pwani, Bi. Roseline Kimaro, alisema kuwa maadhimisho hayo yatatanguliwa na mikutano mbalimbali itakayofanyika kwenye maeneo yenye mikusanyiko ya watu, kwa lengo la kutoa elimu kwa jamii kuhusu haki za watoto na umuhimu wa kuwalinda kwa kushirikiana na wadau, Viongozi wa dini pamoja na Waandishi wa Habari.
Kikao hicho kilihudhuriwa na wawakilishi kutoka taasisi zisizo za kiserikali (NGOs), wadau mbalimbali wa maendeleo kutoka mkoa wa Pwani, Dawati la Jinsia la Police Mkoa, pamoja na baadhi ya watumishi kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa.
Lengo kuu la kikao hicho lilikuwa kuweka mpango mkakati wa pamoja kuhakikisha maadhimisho hayo yanafanyika kwa mafanikio makubwa.
Siku ya Mtoto wa Afrika (African Child Day) huadhimishwa kila mwaka tarehe 16 Juni tangu mwaka 1991, ikiwa ni kumbukumbu ya mchango wa watoto wa mji wa Soweto, Afrika Kusini, waliopaza sauti wakidai elimu bora mnamo mwaka 1976. Katika maandamano hayo ya kihistoria, mamia ya watoto walipigwa risasi na kuuawa, huku zaidi ya watoto 1,000 wakijeruhiwa.
Maadhimisho haya yanalenga kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa elimu bora kwa watoto, utekelezaji wa haki zao za msingi, na kuenzi ujasiri wa watoto wa Soweto waliopigania haki zao katika mazingira magumu.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani
Sanduku la Posta: 30080 Kibaha
Simu ya Mezani: 023 2402287/2402500
Simu ya Mkononi: 023 2402287/2402500
Barua pepe: barua@pwani.go.tz
Hakimiliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Haki zote zimehifadhiwa.