Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Alexander Mkumbo, ameipongeza Mkoa wa Pwani kwa kuibuka kinara wa kitaifa katika uzalishaji wa ajira baada ya kuzalisha ajira 86,621, hatua inayodhihirisha utekelezaji mzuri wa vipaumbele vya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, hususan katika eneo la ajira.
Profesa Mkumbo ametoa pongezi hizo leo wakati wa hafla fupi ya makabidhiano ya hati za mikataba ya uwekezaji kwa wawekezaji waliopatiwa maeneo katika Eneo Maalum la Uchumi la Bagamoyo Eco Maritime City (BEMC SEZ), sambamba na utoaji wa Taarifa ya Hali ya Uwekezaji Nchini kwa mwaka 2025.
“Mhe. Mkuu wa Mkoa, hongera sana. Mkoa wako ndio kinara katika utekelezaji wa kipaumbele cha Mheshimiwa Rais cha uzalishaji wa ajira hapa nchini,” alisema Prof. Mkumbo.
Kwa upande wa miradi ya uwekezaji, Mkoa wa Pwani umeshika nafasi ya pili kitaifa kwa kusajili miradi 208, ukifuatia Mkoa wa Dar es Salaam unaoongoza kwa kusajili miradi 34,000.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi wa Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalum ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA), Gilead Teri, amesema makampuni yaliyokabidhiwa hati za mikataba ya uwekezaji ni Canary Industrials Limited, Grosso Engineering and Fabricators Limited, Jaribu Cashews Production Limited, Novara Global Steel, Shah Steel Global pamoja na MCGA Auto Limited.
Ameongeza kuwa makampuni hayo yanawakilisha uwekezaji katika sekta mbalimbali zenye mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa taifa, ikiwemo viwanda vya chuma, uhandisi, usindikaji wa mazao ya kilimo, pamoja na sekta ya magari na huduma zake.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani
Sanduku la Posta: 30080 Kibaha
Simu ya Mezani: 023 2402287/2402500
Simu ya Mkononi: 023 2402287/2402500
Barua pepe: barua@pwani.go.tz
Hakimiliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Haki zote zimehifadhiwa.