Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhe. Abubakar Kunenge, amesema Mkoa wa Pwani unaendelea kutekeleza kwa vitendo vipaumbele vya Serikali, hususan katika eneo la uzalishaji wa ajira kwa vijana, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kumuunga mkono Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Kunenge ametoa kauli hiyo Januari 05, 2026, wakati wa ziara yake ya kutembelea kongani ya viwanda ya Gaini Company Limited iliyopo Kata ya Kikongo, Wilaya ya Kibaha, mkoani Pwani. Amesema kongani hiyo inatarajiwa kuzalisha ajira zipatazo 1,500 ifikapo mwezi Machi 2026, huku zaidi ya vibarua 300 tayari wakipata ajira katika hatua ya ujenzi wa mradi huo.
Amesema uwekezaji huo unaendana kikamilifu na mkakati wa Serikali wa kukuza uchumi wa viwanda na kuongeza fursa za ajira kwa wananchi, hususan vijana, hatua inayochochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika Mkoa wa Pwani pamoja na kuongeza mapato ya Taifa. Katika hilo, amempongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuvutia wawekezaji na kuweka suala la ajira kuwa kipaumbele cha Serikali.
Aidha, Kunenge amesema Mkoa wa Pwani unaendelea kushirikiana kwa karibu na taasisi wezeshi zikiwemo TANESCO, DAWASA na TANROADS ili kuhakikisha hakuna urasimu unaokwamisha utekelezaji wa miradi ya uwekezaji. Ushirikiano huo unalenga kuhakikisha upatikanaji wa huduma muhimu ikiwemo nishati ya umeme, maji safi na salama pamoja na miundombinu ya barabara.
Ameongeza kuwa mradi wa bomba la gesi kutoka Kinyerezi hadi Chalinze tayari umefanyiwa upembuzi yakinifu wenye thamani ya shilingi bilioni 2.3 na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), jambo litakaloongeza ufanisi wa upatikanaji wa nishati kwa viwanda mkoani Pwani.
Kwa upande wake, Meneja wa Mradi wa kongani hiyo, QS Bradley Cuthbert Muro, amesema ujenzi wa viwanda viwili umefikia hatua za mwisho, ambapo kiwanda cha chuma kimefikia asilimia 85 ya ujenzi huku kiwanda cha cubes kikifikia asilimia 95. Amesema uzalishaji unatarajiwa kuanza rasmi ifikapo mwezi Machi 2026.
Ameongeza kuwa kongani hiyo itajumuisha viwanda vya uzalishaji mkubwa, wa kati na mdogo, ambapo awamu ya kwanza itahusisha viwanda vya uzalishaji mkubwa vitakavyoanza kuzalisha nondo, mabati na mabomba ya chuma ya mraba kuanzia Machi 2026. Alisema ikikamilika, kongani hiyo itakuwa na viwanda vya uzalishaji wa nondo, mabati, steel pipes, hollow sections (RHS, SHS na CHS), flat bars pamoja na misumari.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani
Sanduku la Posta: 30080 Kibaha
Simu ya Mezani: 023 2402287/2402500
Simu ya Mkononi: 023 2402287/2402500
Barua pepe: barua@pwani.go.tz
Hakimiliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Haki zote zimehifadhiwa.