Katibu Tawala wa Mkoa wa Pwani, Rashid Mchatta, amezielekeza Halmashauri ya Mji Rufiji na Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti kuhakikisha kuwa miradi ya maendeleo inakamilika kwa wakati na kuleta tija katika kutatua changamoto za wananchi.
Mchatta alitoa maagizo hayo Leo Juni 19 kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani, wakati wa vikao vya Baraza la Madiwani vilivyofanyika katika halmashauri hizo kwa ajili ya kupitia na kujadili hoja zilizotolewa katika ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa mwaka wa fedha 2024/2025.
Aidha, alizihimiza halmashauri hizo kuimarisha usimamizi wa mapato ya ndani kwa kudhibiti mianya ya upotevu wa fedha, sambamba na kubuni miradi mbalimbali ya maendeleo itakayochangia kuongeza mapato na kuimarisha ustawi wa wananchi.
Vilevile, aliagiza kuhakikisha kuwa hoja zote zilizobaki zinafanyiwa kazi na kufungwa ifikapo Septemba, 2025, na kwamba kusiwe na hoja mpya. Alisisitiza umuhimu wa kuwawezesha wakaguzi wa ndani kuzifunga hoja hizo kabla ya kuwasili kwa mkaguzi wa nje.
Katika kuimarisha ukusanyaji wa mapato, Mchatta alielekeza halmashauri zote kutumia mifumo ya kitaifa ya kidijitali kwa asilimia mia moja (100%) ili kuongeza ufanisi na uwazi katika ukusanyaji na matumizi ya fedha.
Akiwa katika Halmashauri ya Mji Rufiji, aliagiza kuwa mikopo ya asilimia 10 ya mapato ya ndani iendelee kuelekezwa kwenye makundi maalum ili kuwapatia fursa ya ajira na hatimaye kuongeza mapato ya halmashauri.
Pamoja na maagizo hayo, Mchatta alizipongeza halmashauri hizo kwa mafanikio ya ukusanyaji wa mapato na kupata hati safi kwa miaka mitano mfululizo.
Katika hatua nyingine, wenyeviti wa halmashauri hizo walimpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kutoa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo. Pia waliahidi kuhakikisha kuwa hoja zote zilizobaki zitajibiwa kwa wakati.
Naye, Mwakilishi wa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Mkoa wa Pwani, Pastory Massawe, aliwapongeza madiwani kwa usimamizi mzuri uliowezesha halmashauri kupata hati safi kwa miaka mitano mfululizo. Alisisitiza umuhimu wa kuzuia hoja mpya badala ya kuwa na uwezo tu wa kujibu hoja zilizojitokeza.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani
Sanduku la Posta: 30080 Kibaha
Simu ya Mezani: 023 2402287/2402500
Simu ya Mkononi: 023 2402287/2402500
Barua pepe: barua@pwani.go.tz
Hakimiliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Haki zote zimehifadhiwa.