Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhe. Abubakar Kunenge ameipongeza Wakala wa Majengo ya Tanzania TBA kwa juhudi zake za kubuni na kupanga mikakati ya kujenga nyumba za kisasa kwa ajili ya makazi ya wananchi na watumishi wa umma Mkoani Pwani.
Kunenge ametoa pongezi hizo Oktoba 24, 2025 alipokutana na kufanya mazungumzo na ujumbe kutoka TBA uliongozwa na Mkurugenzi wa Miliki Bw. Said Mndeme walipofanya ziara fupi Mkoani Pwani kwa lengo la kufanya ukaguzi wa maeneo wanayomiliki na kujadiliana kuhusu utekelezaji wa mipango ya ujenzi wa nyumba za makazi na upangishaji katika Mkoa huo.
Katika mazungumzo hayo, Kunge amesema hatua hiyo ni muhimu katika kukabiliana na changamoto ya upungufu wa nyumba za kuishi, hasa wakati huu ambapo Mkoa wa Pwani unaendelea kukua kwa kasi kiuchumi na kuwa kitovu cha viwanda nchini.
“Mkoa wa Pwani ni miongoni mwa mikoa inayoongoza kwa uwekezaji wa viwanda nchini, ukuaji huu wa sekta ya viwanda umesababisha ongezeko kubwa la watu wanaohamia kufanya kazi na kuishi katika maeneo mbalimbali ya mkoa, jambo linaloongeza mahitaji ya nyumba bora za makazi,” amesema.
Mkuu huyo wa Mkoa amewahakikishia TBA ushirikiano wa Serikali ya Mkoa wa Pwani katika kuhakikisha miradi hiyo inatekelezwa kwa ufanisi, akisisitiza kuwa Serikali ya Mkoa ipo tayari kutoa usaidizi wowote utakaohitajika ili kuhakikisha malengo ya taasisi hiyo yanafikiwa.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Miliki wa TBA amesema kuwa ziara yao imelenga kukagua na kutathmini maeneo yote yanayomilikiwa na wakala huo ili kuhakikisha yako salama, yanatambulika kisheria na yanatumiwa kwa ufanisi. Ameongeza kuwa TBA inaendelea kuweka mikakati madhubuti ya kuanza miradi ya ujenzi wa nyumba katika maeneo yote inayoyamiliki, kwa lengo la kuongeza wigo wa upatikanaji wa makazi bora kwa watumishi wa serikali na wananchi kwa ujumla.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani
Sanduku la Posta: 30080 Kibaha
Simu ya Mezani: 023 2402287/2402500
Simu ya Mkononi: 023 2402287/2402500
Barua pepe: barua@pwani.go.tz
Hakimiliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Haki zote zimehifadhiwa.