Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhe. Abubakar Kunenge, ametoa wito kwa Bodi ya Kitaifa ya Ushauri wa Msaada wa Kisheria kuongeza juhudi katika kutoa elimu kwa wananchi kuhusu misingi ya haki na sheria, ili kuwawezesha kuelewa haki zao na hatua za kuchukua wanapokutana na changamoto za kisheria.
Mhe. Kunenge alitoa kauli hiyo leo, Juni 24, 2025, alipokutana na wajumbe wa Bodi hiyo wakiongozwa na Mwenyekiti wake, Saulo Malauli, katika kikao kilichofanyika ofisini kwake Kibaha.
“Kutoa elimu ya kisheria ni jambo la msingi litakalowasaidia wananchi kufahamu haki na wajibu wao, kushiriki kikamilifu katika utatuzi wa migogoro na kuepuka matatizo yanayoweza kuzuilika,” alisema Mhe. Kunenge.
Aidha, alishauri Bodi hiyo kushirikiana kwa karibu na wadau wengine wa sekta ya sheria wakiwemo Mahakama, kwa lengo la kubaini maeneo yenye changamoto, kurekebisha sera na sheria zinazohitaji maboresho, na kuhakikisha haki inatendeka kwa kufuata misingi ya maadili na usawa.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Saulo Malauli, alisema kuwa ziara yao inalenga kupata taarifa ya utekelezaji wa msaada wa kisheria mkoani Pwani, kubaini changamoto zilizopo, na kuchukua hatua stahiki ili kuhakikisha huduma hiyo inawafikia walengwa kwa mujibu wa sera na miongozo ya kisheria.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani
Sanduku la Posta: 30080 Kibaha
Simu ya Mezani: 023 2402287/2402500
Simu ya Mkononi: 023 2402287/2402500
Barua pepe: barua@pwani.go.tz
Hakimiliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Haki zote zimehifadhiwa.