Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhe. Aboubakari Kunenge, amekabidhi magari 12 na boti moja vyenye thamani ya shilingi bilioni 7.9 kwa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji mkoani humo.
Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo leo Oktoba 24, 2025, Mhe. Kunenge ameishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Rais wa Awamu ya Sita, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuboresha vitendea kazi vya vyombo vya Ulinzi na Usalama likiwemo Jeshi la Zimamoto na Uokoaji.
Amesema upatikanaji wa magari na boti hizo utaimarisha uwezo wa jeshi hilo katika kutekeleza majukumu yake ya msingi ya kuokoa maisha na mali za wananchi hususan wakati wa majanga ya moto na maafa ya majini.
“Tunamshukuru sana Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuwekeza katika vifaa vya uokoaji. Uboreshaji huu utasaidia kuongeza ufanisi katika kazi za zimamoto na kuimarisha usalama wa wananchi wetu,” amesema Mhe. Kunenge.
Kwa upande wake Kamanda wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Pwani, Jenifa Shirima, amemshukuru Rais na Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kulipa jeshi hilo kipaumbele katika upatikanaji wa rasilimali na vifaa muhimu.
Amesema magari na boti vilivyokabidhiwa vitasaidia kwa kiasi kikubwa katika majukumu ya uokoaji, ikiwemo usafirishaji wa wagonjwa, kudhibiti moto, na kutoa huduma za haraka katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Pwani.
“Vifaa hivi vitasaidia kuongeza kasi ya majibu wakati wa dharura na kupunguza madhara yanayosababishwa na majanga ya moto na ajali. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuona umuhimu wa kuboresha huduma za zimamoto nchini,” amesema Kamanda Shirima.
Upatikanaji wa vifaa hivyo ni sehemu ya juhudi za serikali katika kuhakikisha taasisi za ulinzi na usalama zinakuwa na vifaa vya kisasa vinavyowezesha utoaji wa huduma bora kwa wananchi.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani
Sanduku la Posta: 30080 Kibaha
Simu ya Mezani: 023 2402287/2402500
Simu ya Mkononi: 023 2402287/2402500
Barua pepe: barua@pwani.go.tz
Hakimiliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Haki zote zimehifadhiwa.