Leo, Januari 8, 2026, Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mheshimiwa Abubakar Kunenge, ameendesha kikao kazi maalum cha kutoa muongozo na maelekezo ya utekelezaji wa shughuli za Serikali katika sekta zote mkoani Pwani.
Akizungumza katika kikao hicho, Mheshimiwa Kunenge alisema lengo la mkutano huo ni kuwapa viongozi na watendaji wa Serikali miongozo ya pamoja, akibainisha kuwa Serikali ipo ndani ya siku 100 tangu Rais ateuliwe, hivyo kuna majukumu muhimu yanayopaswa kutekelezwa kwa mshikamano.
“Tumekutana kwa pamoja kwa lengo la kupeana miongozo, kwa kuwa tunafahamu kuwa tupo ndani ya siku mia moja tangu Mheshimiwa Rais ateuliwe, na kuna mambo muhimu yanayotakiwa kufanyika kwa pamoja,” alisema Kunenge
Alisisitiza umuhimu wa kuwa na utekelezaji wa pamoja, mtazamo mmoja na vipaumbele vinavyofanana ili kufanikisha malengo ya maendeleo ya Mkoa. Aidha, aliwataka viongozi na watendaji kufahamu vipaumbele vya Mkoa wa Pwani kwa sasa na kuvitendea kazi ipasavyo.
“Tuna mambo mengi ya kufanya, lakini tunayo vipaumbele ambavyo tukivitekeleza kwa ufanisi vitatuletea tija kubwa zaidi,” aliongeza.
Katika hatua nyingine, Mkuu huyo wa Mkoa amezitaka baadhi ya Halmashauri kuongeza wigo wa mapato ya ndani kwa kubuni vyanzo vipya na kuacha kutegemea vyanzo vya zamani ambavyo havileti tija ya kutosha.
Kunenge pia aliwataka watendaji wote wa Serikali mkoani Pwani kufanya kazi kwa ushirikiano, kupunguza urasimu katika utekelezaji wa majukumu yao na kuhakikisha malengo ya Serikali yanafikiwa kwa wakati. Vilevile, aliwahimiza Waheshimiwa Madiwani kushirikiana na taasisi za umma ili kumuunga mkono Mheshimiwa Rais katika juhudi za kuwaletea wananchi maendeleo.
Kuhusu suala la utawala bora, Kunenge alisisitiza kuwa hakuna mtu aliye juu ya sheria, hivyo ni muhimu kuheshimu mihimili yote mitatu ya dola ili kudumisha haki, uwajibikaji na utawala wa sheria.
Kikao hicho kimefanyika katika Ukumbi wa Destiny uliopo Manispaa ya Kibaha, na kimehudhuriwa na viongozi wakuu wa Mkoa na Wilaya, watendaji wakuu wa Serikali, wawakilishi wa taasisi wezeshi pamoja na Waheshimiwa Madiwani.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani
Sanduku la Posta: 30080 Kibaha
Simu ya Mezani: 023 2402287/2402500
Simu ya Mkononi: 023 2402287/2402500
Barua pepe: barua@pwani.go.tz
Hakimiliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Haki zote zimehifadhiwa.