Leo Juni 6 Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhe. Abubakar Kunenge, leo amepokea jumla ya ng’ombe 300 na mbuzi 2,000 kutoka Taasisi ya Kimataifa ya IDDef yenye makao yake nchini Uturuki, kwa ajili ya kuwawezesha waumini wa dini ya Kiislamu kushiriki ibada ya kuchinja katika Sikukuu ya Iddi El-Adh’ha.
Msaada huo umetolewa kwa lengo la kusaidia waumini katika Mkoa wa Pwani kutekeleza ibada hiyo muhimu ya Kiislamu, kama sehemu ya ibada ya Idd inayoadhimishwa na Waislamu duniani kote.
Akikabidhi rasmi mifugo hiyo kwa Mkuu wa Mkoa, Mwenyekiti wa Taasisi ya IDDef, Bw. Abdul Hamid Khann, alisema kuwa msaada huo umetolewa kama sadaka kutoka kwa Waislamu wa Uturuki, kwa nia ya kushirikiana na wenzao wa Tanzania katika kipindi hiki cha ibada.
Mhe. Kunenge ameishukuru taasisi hiyo kwa mchango huo mkubwa, akibainisha kuwa mifugo yote imekaguliwa na kuthibitika kuwa mizima na inayofaa kwa matumizi ya kitoweo. Aidha, alieleza kuwa Serikali ya Mkoa tayari imeandaa utaratibu maalum kuhakikisha kuwa sadaka hiyo inawafikia waumini wote kwa haki katika maeneo yote ya Mkoa wa Pwani.
Akizungumza kwa niaba ya Sheikh wa Mkoa, Kadhi wa Mkoa wa Pwani, Sheikh Rashid Changunda, aliipongeza IDDef kwa moyo wa upendo na mshikamano waliouonesha, akisema kuwa msaada huo ni baraka kubwa na kielelezo cha udugu wa Kiislamu unaovuka mipaka ya nchi.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani
Sanduku la Posta: 30080 Kibaha
Simu ya Mezani: 023 2402287/2402500
Simu ya Mkononi: 023 2402287/2402500
Barua pepe: barua@pwani.go.tz
Hakimiliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Haki zote zimehifadhiwa.