Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) imeanza utekelezaji wa mpango wa majaribio wa Bima ya Afya kwa Wote, ikiwa ni sehemu ya kutekeleza dhamira ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuhakikisha huduma za afya zinawafikia wananchi wote.
Kauli hiyo imetolewa na Mratibu wa Bima ya Afya kwa Wote kutoka OWM-TAMISEMI, Silvery Maganza, wakati akiwasilisha taarifa katika kikao kazi cha tathmini ya utekelezaji wa ahadi za Rais, hususan katika eneo la Bima ya Afya kwa Wote. Kikao hicho kilifanyika Desemba 18, 2025, katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Kibaha.
Amesema katika utekelezaji wa mpango huo, Serikali imefanya maboresho makubwa kwa kukamilisha kitita cha mafao ya huduma za afya 372 kwa gharama ya shilingi 150,000 kwa mwaka, ikilinganishwa na huduma 277 zilizokuwepo awali.
Aidha, Maganza amesema zoezi la utambuzi wa makundi maalum, hususan wananchi wasio na uwezo, tayari limeanza ili kuhakikisha wanapatiwa huduma za bima ya afya kwa ufanisi. Amesema Serikali imetenga fedha mahsusi kwa ajili ya zoezi hilo, ambapo kila kaya itanufaika na bima ya afya yenye gharama ya shilingi 150,000.
Vilevile, Serikali inaendelea kuboresha upatikanaji wa huduma za afya nchini kwa kuimarisha mifumo ya tiba kwa njia ya mtandao, huduma za uchunguzi wa magonjwa, kuwajengea uwezo wataalam wa afya, kuongeza idadi ya watumishi, kuboresha upatikanaji wa dawa pamoja na kuongeza vituo vya kutolea huduma za afya.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani
Sanduku la Posta: 30080 Kibaha
Simu ya Mezani: 023 2402287/2402500
Simu ya Mkononi: 023 2402287/2402500
Barua pepe: barua@pwani.go.tz
Hakimiliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Haki zote zimehifadhiwa.