Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. George Simbachawene, amempongeza Mkuu wa Mkoa wa Pwani kwa uongozi wake mahiri na namna anavyowashirikisha watendaji wa mkoa katika utekelezaji wa shughuli za Serikali kwa ufanisi.
Akizungumza wakati wa kikao cha tathmini ya utekelezaji wa ahadi za Rais za siku 100, Waziri Simbachawene alisema Mkoa wa Pwani una bahati ya kuwa na kiongozi mwenye uwezo mkubwa wa kiuongozi anayehakikisha watendaji wanashirikishwa kikamilifu katika kazi zao.
“Mna kiongozi mzuri sana mwenye uwezo mkubwa. Kila nikija ananiambia nije nisalimie watu, na ninapofika nakuta watendaji wamejipanga na wanafanya kazi kwa vitendo,” alisema Waziri Simbachawene.
Aidha, Waziri huyo alisisitiza kuwa matarajio ya Serikali ni kuona maendeleo ya mkoa yanaenda sambamba na maendeleo ya wananchi wake. Alieleza kuwa ukuaji wa miundombinu na mazingira unapaswa kuakisi pia ustawi wa maisha ya wananchi wa kawaida.
Alibainisha kuwa utoaji wa huduma za kijamii ikiwemo elimu na afya, pamoja na kuimarisha uchumi wa wananchi na sekta za uzalishaji, ni mambo ya msingi katika kufikia maendeleo jumuishi. Huku akionya dhidi ya kuangalia maendeleo ya viwanda pekee bila kuzingatia manufaa yake kwa wananchi.
“Tusije tukabaki tunaangalia viwanda vinavyozalisha marumaru tukafikiri wananchi wanaguswa moja kwa moja. Ni muhimu kuwaunganisha wananchi kwenye mfumo wa ajira ili waone manufaa ya viwanda hivyo,” alisisitiza.
Kwa mujibu wa Waziri Simbachawene, mafanikio ya maendeleo ya mkoa yataonekana pale ambapo maisha ya wananchi yatakapoboreshwa, ikiwemo uwezo wa kuwapeleka watoto shule, kuendeleza shughuli zao za kiuchumi na kuimarisha ustawi wa familia kwa ujumla.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani
Sanduku la Posta: 30080 Kibaha
Simu ya Mezani: 023 2402287/2402500
Simu ya Mkononi: 023 2402287/2402500
Barua pepe: barua@pwani.go.tz
Hakimiliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Haki zote zimehifadhiwa.