Serikali imewataka Maafisa Habari wa Mikoa na Halmashauri kote nchini kuhakikisha wanatekeleza kikamilifu jukumu lao la kuhabarisha umma kuhusu utekelezaji wa shughuli za maendeleo zinazofanywa na serikali katika maeneo yao.
Wito huo umetolewa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Gerson Msigwa, wakati wa kufunga kikao kazi cha Maafisa Habari wa Mikoa na Halmashauri zote nchini kilichofanyika jijini Dodoma.
Akizungumza katika hafla hiyo, Msigwa alisisitiza kuwa wananchi wanahitaji taarifa sahihi, kwa wakati, na zilizoeleweka kuhusu miradi ya maendeleo, huduma za kijamii, na mikakati mbalimbali ya serikali katika kuwahudumia wananchi.
“Maafisa Habari mnapaswa kuwa sauti ya serikali katika maeneo yenu. Mna wajibu wa kuhakikisha mafanikio ya serikali yanawafikia wananchi, na pia changamoto zinazojitokeza zinaelezwa kwa uhalisia wake,” alisema Msigwa.
Aliongeza kuwa kutowafikishia wananchi taarifa muhimu kunapunguza uelewa na ushiriki wao katika utekelezaji wa sera na mipango ya serikali, hali inayoweza kuchochea upotoshaji au malalamiko yasiyo na msingi.
Serikali, kwa upande wake, imeahidi kuendelea kuwawezesha Maafisa Habari kwa kuwapatia mafunzo, vifaa na teknolojia ya kisasa ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi.
Msigwa pia amewahimiza Maafisa Habari kushirikiana na vyombo vya habari vya kitaifa na vya jamii ili kuhakikisha taarifa za serikali zinafika kwa wananchi kwa njia mbalimbali.
“Nendeni mkaitangaze serikali – taifa linawategemea nyinyi kama daraja kati ya serikali na wananchi,” alisema Msigwa.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani
Sanduku la Posta: 30080 Kibaha
Simu ya Mezani: 023 2402287/2402500
Simu ya Mkononi: 023 2402287/2402500
Barua pepe: barua@pwani.go.tz
Hakimiliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Haki zote zimehifadhiwa.