Kaimu Katibu Tawala Msaidizi wa Utawala na Rasilimali Watu wa Mkoa wa Pwani, Peter Billa, amewataka wazazi, walezi na jamii kwa ujumla kuwa walinzi wa watoto kwa kuhakikisha wanalelewa katika mazingira salama na bora.
Billa ametoa wito huo leo kwa niaba ya Katibu Tawala wa Mkoa wa Pwani, Rashid Mchatta, wakati wa kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika yaliyofanyika kimkoa katika Shule ya Msingi Kambarage, Kata ya Tumbi, Halmashauri ya Kibaha.
"Yote yaliyosemwa hapa leo ni muhimu sana kwa ustawi wa watoto wetu. Mtoto anahitaji ulinzi na mazingira bora ya kuishi. Ni wajibu wetu sisi wazazi, walezi na jamii kuhakikisha hilo linatimia," alisema Billa.
Aidha, aliwasihi wazazi kuepuka migogoro isiyo ya lazima na matumizi ya lugha chafu au vitisho mbele ya watoto kwani hali hiyo huharibu afya ya kisaikolojia ya mtoto na kuathiri mwenendo wake shuleni. Alisisitiza umuhimu wa wazazi kuwa karibu na watoto ili kutambua changamoto zinazowakabili, hususan masuala ya ukatili wa kijinsia.
Billa pia aliwataka wazazi na watoto kushiriki ibada na kuepuka kujihusisha na shughuli zisizofaa mitaani kama vile vibanda umiza, akisisitiza kuwa kushiriki katika imani za kidini hujenga maadili na kuwapa watoto misingi ya kukataa kushiriki vitendo viovu.
Kwa upande wake, Afisa Maendeleo ya Jamii wa Mkoa wa Pwani, Grace Tete, alisema maadhimisho hayo yalitanguliwa na kampeni mbalimbali za kuelimisha jamii kuhusu haki za watoto. Kupitia kampeni hizo, zaidi ya wazazi na walezi 2,000 walifikiwa kwenye maeneo ya masoko mbalimbali mkoani humo.
Aidha, alieleza kuwa Serikali kupitia Mpango wa Taifa wa Kuzuia Ukatili dhidi ya Watoto, imefanikiwa kuwafikia watoto 150 waliopata madhila ya ukatili na kuwapatia huduma stahiki.
Tete alisisitiza kuwa wazazi na walezi wanapaswa kutimiza mahitaji ya msingi ya watoto kama vile chakula, malazi na elimu ili kuwalinda dhidi ya vishawishi hatarishi. Pia alihimiza jamii kuhakikisha mawasiliano bora kati ya watoto na walezi kwa lengo la kujua mapema matatizo yanayowakabili watoto.
Kwa upande wake, Mwakilishi wa Diwani wa Kata ya Tumbi kutoka Chama Cha Mapinduzi (CCM), Bw. Lubawa, aliipongeza Polisi kwa kuimarisha ulinzi na kukabiliana na vitendo vya ubakaji na ukatili wa kijinsia dhidi ya watoto katika kata hiyo.
Nao watoto, kupitia maonesho mbalimbali waliyoyafanya ikiwemo Bunge la watoto, ngonjera, mashairi na risala, waliwasihi wazazi kutimiza majukumu yao ipasavyo, kuepuka migogoro ya kifamilia na kulinda watoto dhidi ya matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii.
Kaulimbiu ya Maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika kwa mwaka 2025 ni "Haki za Mtoto:Tulipotoka, Tulipo na Tuendako”. Kaulimbiu hii inaitaka jamii kutafakari upatikanaji wa haki za watoto tangu zilipoainishwa na Sera ya Maendeleo ya Mtoto mwaka 2008.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani
Sanduku la Posta: 30080 Kibaha
Simu ya Mezani: 023 2402287/2402500
Simu ya Mkononi: 023 2402287/2402500
Barua pepe: barua@pwani.go.tz
Hakimiliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Haki zote zimehifadhiwa.