Katibu Tawala wa Mkoa wa Pwani, Rashid Mchatta, amezielekeza Halmashauri za Bagamoyo na Chalinze kusimamia kwa umakini matumizi ya fedha za umma ili kuepusha hoja zinazotolewa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).
Mchatta alitoa maagizo hayo kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani, katika vikao vya Baraza la Madiwani vilivyofanyika kwenye halmashauri hizo, kwa ajili ya kupitia na kujadili hoja zilizotolewa kwenye ripoti ya CAG kwa mwaka wa fedha 2024/2025.
Katika hotuba yake, Mchatta alizipongeza Halmashauri hizo kwa kufanikisha ukusanyaji wa mapato na kuvuka malengo yaliyowekwa. Aidha, alizitaka kuhakikisha kuwa hoja zote zilizosalia zimefungwa ifikapo tarehe 30 Septemba 2025, sambamba na kuongeza wigo wa mapato kwa kubuni vyanzo vipya vya mapato.
“Imarisheni usimamizi wa mapato ya ndani kwa kudhibiti mianya ya upotevu, kwa mfano kwa kufunga kamera za CCTV katika maeneo kama stendi za mabasi na sehemu nyinginezo zinazohusisha mapato ya moja kwa moja,” alisisitiza Mchatta.
Katika vikao hivyo, Halmashauri ya Bagamoyo na ile ya Chalinze zilipongezwa kwa kupata hati safi kutoka kwa CAG, ikiwa ni ishara ya usimamizi mzuri wa fedha za umma na uwajibikaji wa viongozi wa halmashauri hizo.
Kwa upande wao, wakurugenzi wa Halmashauri hizo walieleza kuwa walifanikiwa kujibu hoja zote zilizotolewa katika ripoti ya CAG, hali iliyosaidia kuimarisha uwazi na nidhamu ya matumizi ya fedha za serikali.
Katika hatua nyingine, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Chalinze, Hassan Mwinyikondo, alisisitiza umuhimu wa kudhibiti mapato ya halmashauri na kuhakikisha matumizi yake yanaendana na bajeti iliyopitishwa, ili kuepusha hoja zisizo za lazima.
Naye Pastory Massawe, Mwakilishi wa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Mkoa wa Pwani, aliwapongeza madiwani kwa kusimamia halmashauri hadi kupata hati safi. Hata hivyo, alisisitiza umuhimu wa kuzuia hoja mpya badala ya kuwa wazuri tu wa kujibu hoja.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani
Sanduku la Posta: 30080 Kibaha
Simu ya Mezani: 023 2402287/2402500
Simu ya Mkononi: 023 2402287/2402500
Barua pepe: barua@pwani.go.tz
Hakimiliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Haki zote zimehifadhiwa.