Katibu Tawala Mkoa wa Pwani, Pili Hassan Mnyema, amekabidhiwa rasmi ofisi leo Juni 27, 2025, kufuatia mabadiliko ya kiutendaji yaliyofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kupitia taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Dkt. Moses Kusiluka, mnamo Juni 23, 2025.
Katika mabadiliko hayo ya uongozi, Pili Mnyema amebadilishana vituo vya kazi na aliyekuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Pwani, Rashid Mchatta, ambaye sasa atahudumu Mkoa wa Tanga.
Hafla ya makabidhiano imefanyika katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Kibaha.
Akizungumza baada ya kupokea ofisi, Mnyema alieleza kushukuru kwa kuendelea kuaminiwa na Mheshimiwa Rais, huku akiomba ushirikiano kutoka kwa watumishi wa Sekretarieti ya Mkoa wa Pwani.
“Ninaomba kwa dhati ushirikiano wenu. Sisi makatibu tawala ni waratibu tu, lakini utekelezaji wa shughuli za kila siku unafanywa na nyinyi. Kazi bila ushirikiano haiwezekani. Nipo tayari kuendelea kujifunza kutoka kwenu na pia kuwafundisha kwa yale niliyojifunza,” alisema Mnyema.
Kwa upande wake, Rashid Mchatta alitoa shukrani kwa uongozi wa mkoa na watumishi wote kwa ushirikiano waliompatia katika kipindi chake cha uongozi kilichodumu kwa miaka miwili na miezi mitatu.
“Nitumie fursa hii kuwashukuru kwa ushirikiano mkubwa mlionipa. Kwa uzoefu wangu, watumishi wa Mkoa wa Pwani mnajituma sana. Naomba muendelee kuonesha ushirikiano huo kwa Katibu Tawala mpya kama mlivyofanya kwangu,” alisema Mchatta.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti wakati wa hafla hiyo, viongozi mbalimbali akiwemo Mkurugenzi wa Halmashauri ya Kibaha, Regina Bieda; Katibu Tawala wa Wilaya ya Mafia, Shabani Shabani; Mkuu wa Kitengo cha Ukaguzi wa Ndani kutoka Sekretarieti ya Mkoa, Obadia Malima; na Meneja wa TRA Mkoa wa Pwani, Masawe Masawe, waliwapongeza viongozi hao kwa kuaminiwa na Mheshimiwa Rais, huku wakiahidi ushirikiano wa karibu kwa Katibu Tawala mpya katika kutekeleza majukumu ya serikali kwa manufaa ya wananchi wa Mkoa wa Pwani.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani
Sanduku la Posta: 30080 Kibaha
Simu ya Mezani: 023 2402287/2402500
Simu ya Mkononi: 023 2402287/2402500
Barua pepe: barua@pwani.go.tz
Hakimiliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani. Haki zote zimehifadhiwa.